Home » » ZOEZI LA SENSA LAINGIA DOSARI MATEMBWE, WALEVI, WAZURURAJI WAKAMATWA

ZOEZI LA SENSA LAINGIA DOSARI MATEMBWE, WALEVI, WAZURURAJI WAKAMATWA


Mwandishi wetu, Njombe Yetu
Zoezi la sensa ya watu na makazi mwaka 2012 linaloendelea nchi nzima limeingia dosari katika kijiji cha Matembwe kilichopo tarafa ya Lupembe Mkoani Njombe kutokana na baadhi ya wananchi kukimbia makazi yao.
Wananchi hao wamekimbia makazi yao kutokana na baadhi ya wanakijiji kukamatwa kwa kosa la uzururaji na kunywa pombe muda wa kazi jambo ambalo wanakijiji hao walilihusisha na zoezi la sensa.
“Kuna baadhi ya watu baada ya kuona makarani wa sensa hawafiki katika makazi yao kama walivyotarajia waliamua kutafuta sehemu ili kuwasubiri wawahesabu, wakaenda kukaa kilabuni na kuanza kunywa pombe, askari wa Lupembe wakawakamata” alisema mmoja wa wanakijiji wa Matembwe.
Kutokana na wananchi wengi kutouelewa vizuri utaratibu wa uendeshaji wa sensa ya mwaka huu, wengi wamejikuta wakiwa njiapanda na kushindwa kujua namna wanavyotakiwa kushiriki katika zoezi hilo, jambo lililochangia wengine kukaa vijiweni wakingoja makarani kuwahesabu hapo.
Baadhi ya watu waliokamatwa na askari kutokana na kukaa vijiweni na kunywa pombe muda wa kazi wameeleza kuwa waliambiwa walipe faini kati ya shilingi elfu ishirini na elfu hamsini. 
Hata hivyo wananchi hao walilalamika kuwa pesa hizo zinazodaiwa kuwa ni faini zililipwa katika ofisi bubu hivyo kudhani wamefanyiwa uhuni.
“Wananchi wengine wameamua kukimbia zoezi la sensa kwa kudhani mwenyekiti wa sensa wilaya ndiye aliagiza wenzao wakamatwe na kuhisi ni uonevu umefanyika kwani waliokamatwa walikuwa wanasubiri kuhesabiwa kama wengine” alisema mwanakijiji huyo ambaye hakutaka jina lake liandikwe.
Zoezi la sensa linaloendelea nchini sasa hivi limekuwa linakumbwa na vikwazo kadhaa ikiwemo madai ya ukosefu wa vifaa kama vile madodoso na baadhi ya makarani kususia kazi yao kutokana na madai ya posho yao huku wengine wakigomea kwa sababu za shinikizo na itikadi za kidini na kisiasa
Blogzamikoa

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa