Home » » WASIOCHUKUA RISITI BAADA MANUNUZI KUFIKISHWA MAHAKAMANI.

WASIOCHUKUA RISITI BAADA MANUNUZI KUFIKISHWA MAHAKAMANI.


Na Festus Pangani, Ludewa-Njombe Yetu
MKUU wa Wilaya ya Ludewa katika Mkoa wa Njombe Juma Solomoni Madaha amemtaka Mkuu wa Kituo cha Polisi Wialya kumkamata mtu yeyote atakayepatikana au kununua bidhaa dukani bila kuwa na risiti.
Madaha alitoa agizo hilo hivi karibuni katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye stendi ya mabasi yaendayo Manda na Njombe ambapo pamoja na mambo mengine aliutumia mkutano huo kwa kujitambulisha kwa wananchi wa vijiji vya Ludewa (M) Ludewa (K) vinavyounda kata ya Ludewa.
Kauli ya mkuu huyo wa wilaya imekuja baada ya kugundua kuwa serikali inakosa mapato kwa sababu ya wafanyabiashara wasio waaminifu ambao wamekuwa wakiuuza bidhaa bila kutoa risiti jambo linaloikosesha serikali mapato ingawa hakusema ni kwa kiasi gani serikali inakosa mapato kwa mwezi.
Ni kutokana na ukwepaji huo wa kodi akaliagiza jeshi la polisi wilayani humo kumkamata mtu yeyote atakayeonekana kabeba bidhaa isiyokuwa na risiti na kumfungulia mashtaka mahakamani na kutaja duka alilonunua bidhaa hiyo.
Aidha aliwaagiza wafanyabiashara wa bidhaa mbalimbali kuacha tabia ya kukwepa kodi kwa kugushi vitabu vinavyoshindwa kutoa mwongozo kwa maafisa mapato (TRA) kushindwa kumkadilia kodi mfanyabiashara jambo linaloisababishia serikali kukosa mapato.
Awali akitoa taarifa Onesmo Haule ambaye ni afisa mtendaji wa kata ya Ludewa yenye wakazi 10,195, alisema kata yake inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo uhaba wa maji safi na salama, barabara mbovu za mitaa, kuchelewa kwa mbolea ya ruzuku na ulimaji wa mahindi mjini.
 Kwa upande wa elimu Haule alisema kuwa kata yake inazo shule za msingi tano na sekondari tatu ikiwemo chief kidulile inayomilikiwa na serikali, St Alois inayomilikiwa na kanisa Katoliki na Ludewa sekondari inayomilikiwa na jumuia ya wazazi wa ccm. Na kwamba shule zote zinakabiliwa na upungufu wa walimu, vitabu na matundu ya vyoo.
Blogzamikoa

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa