HASSAN MAAJAR TRUST YAKABIDHI MADAWATI 680 KWA RC WA NJOMBE.



 Mkuu wa mkoa wa NjombeKaptain Mstaafu Asseri Msangi katika picha ya pamoja na baadhi ya wanafunzi.

 Mkuu wa mkoa wa Njombe Kaptain Mstaafu Asseri Msangi (aliyekaa wa pili kushoto), Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi Hassan Majaar Trust Bi. Zena Maajar Tenga (waliosimama wa pili kushoto) na Mwakilishi kutoka Kampuni ya Tigo pamoja na baadhi ya Walimu na Wanafunzi wakiwa katika picha ya ukumbusho.

Wanafunzi wakionyesha furaha baada ya kuboreshewa mazingira ya kusoma na Taasisi ya Hassan Maajar Trust ambayo lengo lake ni kutatua tatizo la Madawati nchini na kuhakikisha kauli mbiu yao ya “Dawati kwa kila mwanafunzi” inatimia.

MAFUTA YA PETROLI YAADIMIKA MKOANI NJOMBE

Festus Pangani, Njombe Yetu
Kwa siku ya tatu sasa mji wa Njombe umekumbwa na adha ya kukosekana kwa nishati ya mafuta ya petroli kwenye vituo vya mafuta hali inayopelekea kukwama kwa usafiri na kushuka kwa uchumi miongoni mwa jamii.
Hali hiyo imetokea kuanzia septemba 30 mwezi uliopita hadi sasa ambapo hadi hii leo ni kituo kimoja tu cha mafuta cha Ndime PetrolSstation kinauza mafuta hayo.
Wakizungumza na Njombe Yetu kwa nyakati tofauti baadhi ya madereva wa magari na pikipiki mjini Njombe wamesema kuwa adha hiyo imepelekea baadhi ya magari na pikipiki kuzima njiani yakiwa na abiria kitu ambacho kimeleta usumbufu kwa abiria.
Kwa upande wao mameneja wa baadhi ya vituo vya mafuta mjini hapa Prosper Mtewelewa wa kituo cha Ndime Petrol Station na Kaimu Meneja wa kituo cha mafuta cha Total wamesema tatizo hilo limetokea sehema ya kusambazia mafuta kutokana na siku za jumamosi na jumapili kutokuwepo kikazi.
Hata hivyo pamoja na kutokuwepo kwa mafuta mjini Njombe hakuna ongezeko lolote la bei ya mafuta mkoani hapa.
Blogzamikoa

TANESCO NA MWEKEZAJI KUTOKA MAREKANI KUZALISHA UMEME MEGAWATI 400

Na Festus Pangani, Njombe Yetu
Serikali ya Tanzania kupitia shirika la umeme tanesco kwa kushirikiana na mwekezaji kutoka nchini marekani, inajiandaa kutekeleza mradi wa umeme wa maji katika mto ruhuji.
Akizungmza wakati wa baraza la madiwani Mpimaji ardhi   mwandamizi wa Tanesco makao makuu Hamis Boby amesema mradi huo unatarajiwa kukamilika hadi kufikia mwaka 2019 na kuzalisha umeme wa megawati takribani mia tatu hadi mia nne.
Boby amesema mradi huo utahusisha ujenzi wa mgodi kufua  umeme wa megawati 350 hadi 400, bwawa la kuhifadhi maji, bwawa la kuzalisha umeme, njia ya umeme, barabara, njia ya kusafirisha maji chini ya ardhi, ofisI na makazi.
Hata hivyo amesema hatua hiyo itazingatia haki za wananchi katika eneo husika kwa kulipwa fidia ya ardhi, kupata huduma za kijamii, elimu ya mahusiano, pamoja na huduma nyingine zitakazopendekezwa kwenye makubaliano yao na wadau.
Kwa upande wao madiwani wa halmashauri ya mji wa Njombe na wilaya ya Njombe wameupongeza mpango huo wa serikali na kuwataka wawekezaji hao kutoa fidia kwa wananchi watakaohamishwa ili kupisha utekelezaji wa mradi huo bila ubaguzi wala upendeleo.
Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Ludewa Venancy Kabelege amewataka madiwani kushirikiana na serikali katika kuwahamasisha wananchi ili kufanikisha zoezi hilo la mradi.
Blogzamikoa

KATIBU MWENEZI WA CHADEMA MAKETE HASOMEKI......


Mwenyekiti  wa Chadema Taifa Mhe. Freeman Mbowe

Katika hali ambayo haikutegemewa na wengi, katibu wa itikadi na uenezi wa CHADEMA wilayani Makete Bw. Sinene amekifagilia chama cha mapinduzi kwa kusema kuwa kimejitahidi katika mambo yake ikiwemo kuwa na wanachama wengi wilayani hapo kwa zaidi ya asilimia 90

Sinene ameyasema hayo alipokuwa akitoa nasaha zake alipoalikwa kuhudhuria mkutano wa uchaguzi wa CCM uliofanyika jana kwenye ukumbi wa shule ya sekondari Iwawa wilayani hapo

Katibu huyo alisema “nikilinganisha huko nyuma na hii leo kwa kweli chama chenu kimejitahidi kwa zaidi ya asilimia 90, mna wanachama wengi na mnaendelea kufanya mengi”

Awali wakati akianza kutoa salamu zake alisema unapokwenda sehemu inabidi utumie taratibu za eneo hilo, hivyo kulazimika kusema ‘CCM hoyeeeeeee’ hali iliyowafurahisha wajumbe wa mkutano huo wakiwemo viongozi wa CCM

Baada ya kumaliza salamu zake hizo kulipelekea utani wa hapa na pale ikiwemo kumvalisha kofia ya CCM ingawa alikataa kuivaa huku wengine wakitaka kumpa shati la kijani, na sauti za kumkaribisha CCM zikisikika

Akizungumza mara baada ya kiongozi huyo wa CHADEMA kumaliza kutoa salamu zake, katibu wa CCm wilaya ya Makete Miraji Mtaturu alisema ni kweli chama chake ni kikubwa na wapinzani watazidi kupata tabu kama alivyokiri mwenyewe

“Ndugu wajumbe kauli ya katibu mwenezi wa CHADEMA mmeisikia wenyewe, kwa kawaida katibu mwenezi ni msemaji wa chama, hivyo kauli yake ni kauli ya chama, nachopenda kumwambia hakuna haja ya kupoteza muda, njoo CCM ndugu yangu” alidai Mtaturu

Kauli hiyo ya katibu mwenezi wa CHADEMA ilizua gumzo miongoni mwa wanachama wake waliokuwa nje ya ukumbi huo huku wakisikika wakisema amejimaliza kisiasa na kuona hana haja ya kuendelea kuwepo ndani ya Chadema na badala yake ahamie CCM aliyoifagilia

Kauli hiyo pia ilitumiwa na wagombea wa CCM katika uchaguzi huo hasa wale waliokuwa wakitetea nafasi zao akiwemo Mzee Mwamwala kwa kusema kuwa “katika uongozi wangu nimefanya mengi mazuri hadi mmesikia mwenyewe CHADEMA wanaikubali CCM na wasingeikubali bila uongozi wangu mahiri, hivyo naomba kura zenu”

Pamoja na kutumia fursa hiyo Mzee Mwamwala alishindwa kutetea kiti chake na nafasi yake ilichukuliwa na Francis Chaula aliyepata kura 791 dhidi ya Mwamwala aliyepata kura 155
Francis Godwin Blog

Diwani CCM aliyejeruhiwa sasa ahamishiwa Muhimbili



  *Pia wamo Samia na Dk. Mwinyi
Diwani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Kata ya Ramadhani, Wilaya ya Wanging’ombe mkoa wa Njombe, Livingstone Luvanda, ambaye alijeruhiwa vibaya kwa kupingwa na mgombea wa nafasi ya Katibu wa Siasa na Uenezi wa wilaya hiyo, amehamishiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) kwa matibabu zaidi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe, Fulghence Ngonyani, akizungumza na NIPASHE jana alisema diwani huyo amehamishiwa katika hospitali hiyo kutoka Hospitali ya Mkoa ya Kibena alikokuwa amelazwa awali.

Mgombea huyo ambaye anagombea nafasi ya Katibu wa Itikadi na Uenezi wilaya ya Njombe (jina tunalihifadhi), alimpiga diwani huyo kutokana na misuguano ya kiasa kwa madai kuwa  diwani huyo alikuwa kikwazo kwake ili asiweze kuchaguliwa ambapo sasa anashikiliwa na jeshi la polisi.

Awali diwani huyo akizungumza na gazeti juzi  akiwa amelazwa katika Hospitali ya Kibena,  alisema alivamiwa  majira ya saa 5:30 asubuhi wakati akitoka nyumbani kwake kuelekea katika Shule ya Kimataifa ya Mchepuo wa Kiingereza ya Livingstone kuhudhuria mahafali.

Luvanda alisema akiwa hatambui kinachoendelea, ghafla alivamiwa na mgombea huyo  na kuanza kumpiga kwa kutumia stuli hali iliyomfanya aanguke chini na kupoteza fahamu papo hapo.



Luvanda alisema kabla ya kupata mkasa huo, alidai mgombea huyo alimtumia ujumbe mfupi wa maneno (sms)  katika simu yake ya  mkononi akimweleza kuwa nilazima atamuua kutokana na kumuwekea vikwazo  ili asichaguliwe katika nafasi anayoomba.

Hata hivyo, wakati tunakwenda mitamboni, taarifa zilizopatikana zilieleza kuwa mgombea huyo alifikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Njombe kwa kosa la kumjeruhi diwani huyo ambapo amerudishwa mahabusu baada ya kukosa wadhamini hadi Oktoba 2, mwaka huu kesi hiyo itakaposikilizwa tena.
CHANZO: NIPASHE

Bweni la wanafunzi lawaka moto Njombe



Zaidi ya wanafunzi 93 wa kidato cha tatu na nne katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Wanike mkoani Njombe, wamenusurika kifo baada ya bweni lao kuteketea kwa moto.


Mkuu wa Wilaya ya Wang’ing’ombe, Esterina Kilasi, alisema tukio hilo lilitokea Septemba 13, mwaka huu saa 4:00 usiku.


Alisema moto huo uliteketeza vifaa mbalimbali  vya wanafunzi.

Hata hivyo, alisema moto huo hakuleta madhara kwa upande wa wanafunzi na thamani ya vifaa pamoja na chanzo cha moto huo havijafahamika.

CHANZO: NIPASHE

MWENYEKITI MPYA WA CCM LUDEWA AAHIDI MAKUBWA KWAVIJANA

Festus Pangani, Njombe Yetu.

Mwenyekiti wa vijana kupitia Chama Cha Mapinduzi wilayani Ludewa Bi.Elizabeth Augustino Haule ameahidi kufanya mambo makubwa kwa vijana baada ya kumchagua kuwa mwenyekiti kwa kipindi cha miaka mine.

 Akizungumza na waandishi wa habari jana Bi. Elizabeth alisema kutokana na yeye kuwa mjasiliamali atatumia fulsa hiyo kwa kushirikiana na wadau wengine wilayani humo kutoa elimu ya kujitambua kwani vijana walio wengi bado hawajitambui.

 Alisema kijana anapaswa kijiajiri na si kusubiri kuajiriwa kwa maisha bora kwa kila mtanzania hayaji kwa kutofanya kazi na kusubiri mtu au kampuni ianzishe ndipo uajiliwe.

Elizabeth alibainisha kuwa mafanikio yake mpaka alipofikia kuwa mwenyekiti ni juhudi binafsi na si mtu alikuwa nyuma yake kwani katika mikakati yake ilikuwa kuwa diwani wa viti maalumu lakini bado lengo hilo halijafikiwa na hajakata tamaa kwa hilo.

Aidha amewataka vijana wa Chama Cha Mapinduzi kutokukubali kurubuniwa na wanasiasa kwa kuwa mgongo wao bali kuzingatia kanuni na sheria za chama hicho katika kuwapata viongozi bora na kuendeleza juhudi za kukijenga chama.

Bi.Eliza alisema vijana kwa sasa wanahitaji elimu ya ujasilia mali na mitaji na si vinginevyo hivyo kama itaanzishwa Bank ya vijana itakuwa ukombozi mkubwa kwani vijana wengi wataweza kupata mitaji na kufanya biashara zao.

Aliwaasa vijana wa wilaya ya Ludewa kutobweteka badala yake kujituma katika kazi mbalimbali kwani kupitia migodi ya Mchuchuma na Liganga vijana wa Ludewa wataweza kujikwamua kiuchumi na kuendesha maisha yao bila hofu.

Bi.Elizabeth alisema vijana wengi nchini wamekuwa ni watu wa kulalamika badala ya kufanya kazi hiyo si busala kwani maisha bora kwa kila mtanzania hayaji kwa malalamiko bali kwa kujitambua katika ufanyaji kazi za kujiongezea kipato.

Blogzamikoa

SEKTA YA UTALII NJOMBE IMETELEKEZWA?

Na Festus Pangani, Njombe Yetu
Sekta ya utalii katika mkoa wa Njombe imesahaulika licha ya kuliingizia taifa kipato kutokana na wageni mbalimbali wanaotembelea vituo vya utalii kwa ajili ya kujionea maajabu mbalimbali katika vivutio hivyo.

Mkoa wa Njombe unavivutio vingi vya utalii, ikiwamo hifadhi ya wanyama ya kitulo, shamba la maua yenye kuvutia na kustaajabisha lililopo Uwemba na mwamba wenye ramani ya afrika unaopatikana katika Kijiji cha Igodiva Tarafa ya Imalinyi wilayani Wanging’ombe.

Hata hivyo kutokuwapo kwa juhudi za kutosha katika kuhamasisha wananchi kutembelea vivutio hivyo kumechangia vivutio vingi vya utalii kutofahamika hata kwa baadhi ya wenyeji wa mkoa wa huo.
Akizungumza na Blogzamikoa Afisa Utalii, Maliasili na Mali kale wa Wilaya ya Njombe Abed Henry Chaula alikiri kuwa  wakazi wa mkoa wa Njombe kutokuwa na mwamko wa kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo mkoani hapa hali ambayo inachangia kutofahamika kwa vivutio hivyo.
“Baadhi ya wakazi wengi wa mkoa huu hawana mwamko wa kutembelea vivutio vya utalii kwa kuzani kuwa anayepaswa kutembelea vivutio hivyo ni watalii kutoka nje ya nchi pekee, lakini wengine wako hapa mkoani hawajui vivutio vya utalii vilivyopo mkoani hapa wakiamini kuwa fursa ya utalii ipo katika mikoa ya kusini pekee,” alisema Chaula.

Chaula alikiri kutofanya jitihada za makusudi katika kuvitangaza vivutio vya utalii vilivyopo mkoani hapa pamoja na kutoa hamasa ya kutosha kwa wananchi hususani wenyeji wa mkoa wa Njombe kutembelea vivutio hivyo vya utalii.

Hata hivyo alitoa wito kwa wananchi wa mkoa huo kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio vya utalii ili kuwa mabolozi wazuri wa vivutio hivyo.
“Nawaomba wakazi wa Njombe kuwa na utaratibu wa kutembelea vituo vya utalii, unajua ni aibu mgeni anakuja anakuuliza kivutio cha utalii kilichpo katika eneo lako halafu mwenyeji hukijui,’’ alisema.
Chaula alisema kukua kwa sekta ya utalii katika mkoa kutasaidia kupatikana kwa fursa nyingi za ajira na hivyo kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira nchini.
Baadhi ya vivutio vya utalii vilivyopo katika mkoa wa Njombe ni pamoja na mapango na misitu ya nyumba nitu, mwamba wenye ramani ya afrika wenye ukubwa wa hekari  saba, mpanga kipengele, hifadhi ya Kituro na Mdandu ambako kunapatikana boma la Wajerumani na mahakama ya mwanzo iliyojengwa na wajerumani pamoja na mti mkubwa wa asili wa Mlizombe.
Blogzamikoa

BWENI LATEKETEA KWA MOTO NJOMBE, WANAFUNZI 93 WANUSURIKA KIFO

Festus Pangani, Njombe Yetu
WANAFUNZI 93 wamenusurika kufa baada ya bweni lao kutekea kwa moto usiku wa kuamkia leo katika shule ya sekondari ya wasichana ya Wanike iliyopo Kata ya Mdandu wilaya ya Wanging'ombe Mkoani Njombe.

Mkuu wa wilaya hiyo Bi. Estelina Kilasi amesema, tukio hilo limetokea septemba 13 saa 4 usiku na kuteketeza vifaa mbalimbali vya wanafunzi hao ambavyo thamani yake bado haijajulikana na chanzo cha moto huo hakijafahamika.aa

Bi Kilasi amsema, bweni ambalo limeteketea ni la wasichana wanaosoma kidato cha tatu na cha nne ambao wote walifanikiwa kutoka nje na kuacha mali zao zikiteketea kwa moto.

Amevitaja vitu hivyo kuwa ni pamoja ni daftari, vitanda, magodoro na nguo za kiraia na sare zao vyote vimeteketea kwa moto huo.

Kutokana na ajali hiyo Mkuu huyo wa wilaya ameagiza wazazi wote kufika shuleni hapo septemba 16 ili kujadili kwa pamoja kuhusiana na tatizo hilo.
Blogzamikoa

NJOMBE MEDIA CLUB YAZINDULIWA





Mwandishi wetu, Njombe Yetu
Septemba 11, mwaka huu jamii ya Wananjombe ilishuhudia uzinduzi wa jumuiya ya wanahabari Njombe ambayo inajulikana kwa jina la Njombe Media Club itakayokuwa ikiwaunganisha wanahabari na wadau wa habari wa mkoani humo.
Lengo la kuanzishwa kwa club hiyo ya kutetea maslahi ya wanahabari Njombe na kuwekana sawa katika kahakikisha tasnia ya habari mkoani hapa inakua na kuchangia katika maendeleo.
Pamoja na kwamba mkoa wa Njombe umeanzishwa muda kidogo uliopita, klabu hii ya waandishi imeanzishwa sasa hasa kwa msukumo wa mauaji ya mwandishi wa kituo cha Channel Ten Iringa, Daudi Mwangosi aliyeuawa kijiji cha Nyololo wilayani mufindi katika shughuli ya kisiasa ya Chadema.
Klabu hiyo ya wanahabari mkoani Njombe imejumuisha wadau na wanahabari kutoka vituo mbalimbali vya habari kama vile gazeti la Kwanza Jamii – Njombe, Radio Uplands – Njombe, Best FM Ludewa, Kitulo FM na wawakilishi wa vituo mbalimbali vya redio na televisheni za kitaifa mkoani hapa na waandishi binafsi.
Pamoja na mambo mengine, wajumbe wa Njombe Media Club walitoa maoni yao kwa namna tofauti kuhusiana na mauaji ya Mwangosi na hatimaye klabu kutoa tamko rasmi na mtazamo kuhusiana na tukio hilo na mengine yanayofanana na hilo.
Bazil Makungu ambaye ni Mwenyekiti wa Njombe Media Club alisema “Nimesikitishwa na tukio zima, inasikitisha kuona uongo unaendelea kuenezwa wakati ukweli upo wazi na kila mtu anaona kupitia picha na video. Nina laani kitendo hicho na matumizi ya silaha zamoto si suluhu ya matatizo katika Jamii”
Naye Simon Mkina akichangia maoni yake alisema “Uandishi wa habari ni taaluma inayotakiwa kuheshimiwa, tufungue ukurasa mpya, Njombe inatakiwa kuwa na chama chenye nguvu  na umoja ambao utahakikisha usalama kwa waandishi. Kwa kuwa na umoja wenye nguvu waandishi watajiimarisha kiuchumi, tutakuza taaluma na kupata fedha kutoka kwa mashirika mengine”
Tamko la Njombe Media Club kuhusu mauaji ya mwandishi ni kuwa “Kwa suala la mwangosi, ni wazi kwamba alikuwa ni mwandishi jasiri . kifo chake kimekuwa cha kinyama sana kiasi kwamba ni ngumu kuelezeka mdomoni. Natoa pole kwa familia, waandishi wote na kwa wananchi wote kwa ujumla”
 Blogzamikoa

UJENZI WA BARABARA ZA MITAA KWA KIWANGO CHA LAMI NJOMBE WAANZA KWA KASI













Ujenzi huo unatarajiwa kukamilika miezi sita kutoka sasa kwa kiwango cha lami. Ujenzi huo unaanzia eneo la soko la wakulima karibu na ofisi za CCM wilaya na barabara ya mtaa wa Kongo
Blogzamikoa

NJOMBE KUANZA KUSAMBAZA PEMBEJEO

Festus Pangani, Njombe
Wakati msimu wa kilimo ukiwa umeanza kwa baadhi ya mikoa hapa nchini, tayari serikali imeanza kusambaza vocha za  ruzuku za pembejeo kwa wakulima ili kwenda sanjari na msimu  wa kilimo.
Mwenyekiti wa kamati ya pembejeo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Njombe Sara Dumba amesema wilaya ya Njombe ni miongoni mwa wilaya ambazo tayari zimepokea vocha hizo huku wakitarajia kuanza kuzisambaza kwa wakulima ambao shughuli za kilimo huanza mapema katika maeneo yao.
Akielezea mchakato wa kufikisha vocha za pembejeo kwa wakulima  Dumba amesema hatua za kuwafikishia wakulima hao zinafanyika huku akieleza kuwa  zoezi hilo kwa mwaka huu linafanywa na serikali kwa kuyatumia makampuni ambayo yatatafuta mawakala watakaofanya kazi ya usambazaji.
Aidha mwenyekiti huyo wa kamati ya vocha za pembejeo amesisitiza kuwa pembejeo hizo lazima ziwafikie walengwa na si vinginevyo.
blogzamikoa

SAKATA LA KUHAMISHWA MTENDAJI IGWACHANYA, WANANCHI WAMTAKA MTENDAJI WAO

*RC amtetea DC kuhamia Mdandu
Na Waandishi wetu
Wananchi wa Kata ya Igwachanya wanamlilia aliyekuwa Mtendaji wa Kata yao kwa maelezo kuwa alikuwa mchapakazi.
Taarifa ambazo Kwanza Jamii-Njombe imezipata zinasema Job Fute amehamishwa kutoka katika kata hiyo kimyakimya baada ya kulitaarifu gazeti hili juu ya tetesi zilizopo katika kata hiyo juu ya uamuzi wa Mkuu wa Wilaya ya Wanging’ombe kutokubali nyumba ya mbunge na kuamua kuanzia shughuli zake kata ya Mdandu.
Imefahamika baada ya Fute kuondolewa katika wadhifa wake kama mtendaji wa Kata ya Igwachanya, hivi sasa yupo mapokezi katika idara ya utumishi katika ofisi za Halmashauri kama adhabu.
Hata hivyo, katika mkutano na wananchi, Mkuu wa Mkoa wa Njombe Kepteni (Mstaafu), Assery Msangi aliwaeleza wananchi wa Igwachanya kuwa, kitendo cha kuamua kutumia ofisi za Mdandu ni kuepuka matumizi mabaya ya fedha kwani ingeigharibu wilaya hiyo ya Wanging’ombe kiasi kisichopungua sh. 90 milioni kuikarabati shule waliyokuwa wamepewa na kanisa huko Igwachanya.
Msangi aliyetumia muda mwingi kuelezea kwa nini ofisi ya DC alisema “Maneno yamekuwa mengi, sasa ni wakati wa kufanya kazi…tumeshatengewa sh.2.5 bilioni kwa ajili ya kujenga ofisi.”
Hata hivyo aliwataka wakazi hao kukubali madhara yanayotokana na eneo lao kuwa makao makuu kama kubomolewa nyumba kutokana na upanuzi wa barabara na pamoja kuanza kulipia huduma kama maji.
Akizungumzia uhamisho wa ghafla wa mtendaji wa kata ya Igwachanya kwa kueleza ‘ukweli’, Shukuru Martin, mkazi wa eneo hilo amesema, muda mfupi wa Fute umekuwa na maendeleo ya haraka hasa uhamasishaji wa uchangiaji wa sekondari.
Alikwenda mbele na kuongeza, wakazi wa eneo hilo hawaoni jambo baya aliloeleza kwenye gazeti na kuongeza; “tunashangaa serikali ilivyokuja juu na kumwamisha kiongozi wetu tena bila hata kutuambia lolote. Sasa tutaona itakavyokuwa sababu hatutamkubali mtendaji yoyote atakayeletwa kwenye kata hii.”
Naye Athuman Kilamlya, mkazi wa Igwachanya amesema, uamuzi huo unaonesha pasipo shaka kwamba, serikali haiwapendi viongozi wanaopenda kusema kama taarifa za Fute alizotoa kupitia Kwanza Jamii-Njombe.
Hildegat Mwanyika alilaumu kitendo cha mkurugenzi kumhamisha ghafla mtendaji huyo bila kuangalia upande wa pili ambao ni wa wananchi kwani wanamjua utendaji wake na kumwondoa ni sawa na kuwarudisha wananchi nyuma kimaendeleo.
“Mkuu wa wilaya alibisha hodi hapa na tulimpokea kwa moyo mmoja sasa kwanini aondoke tena bila taarifa yoyote? Mtendaji aliongea kwa niaba yetu sasa kwanini mkurugenzi amwamishe bila hata kusikia lolote kutoka kwetu, kwa maana hiyo mkurugenzi pia hana nia njema na sisi na anakubaliana na yale ambayo yataendelea kuturudisha nyuma,” alisisitiza.
Igwachanya ni eneo lililopo Wanging’ombe na Rais Jakaya Kikwete alitangaza kuwa litakuwa makao makuu ya wilaya. Kutokana na maandalizi duni ya kulifanya eneo hilo kuwa makao makuu, Mkuu wa wilaya hiyo, Esterina Kilasi aliamua kuweka ofisi eneo ya Mdandu kwa muda, jambo lililowatisha wakazi wa Igwachanya kuwa huenda alitaka kuhamia huko moja kwa moja.
Chanzo: Jamii Kwanza Njombe

MUONEKANO WA GAZETI LA 'KWANZA JAMII NJOMBE' TOLEO LA SEPTEMBA 3-19,2012

WAWILI MBARONI KWA KUKATAA KUHESABIWA MAKAMBAKO

Festus Pangani, Njombe Yetu
Jeshi la Polisi Mkoani Njombe linawashikilia watu wawili Athuman Saidi Kivanga Mkazi wa Mtaa wa Kawawa Mji wa  Makambako na Yasini Shaibu wa Kijiji cha Kipagamo Kwa Tuhuma za Kukataa Kuhesabiwa.
Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoani  Njombe ACP Fulgency  Ngonyani Amesema Watu Hao Wamekatwa Agosti 27 Mwaka Huu Majira ya Saa Tano Asubuhi Ambapo Watuhumiwa Hao Walikataa Kuhesabiwa Kwa Madai Kuwa Imani Zao Haziruhusu Kufanya Hivyo.
Kamanda Ngonyani Amesema Kitendo cha Kukataa Kuhesabiwa ni Kosa la Jinai na Kinyume cha Sheria na Kwamba Watuhumiwa Wamekamatwa Kwa Mahojiano Ikiwa ni Pamoja na Kuwaelimisha Juu ya Umuhimu wa Sensa na Endapo Watazidi Kukataa Watafikishwa Mahakamani.
Katika Tukio Jingine Kamanda Huyo Amesema Watu Wasiofahamika Wamevunja Nyumba ya Fredy Mtulua Mkazi wa Kijiji Cha Igagala Wilaya ya Wanging'ombe na Kuiba Pikipiki Moja Aina ya Skymark Yenye Namba za Usajili T 664 BNQ Yenye Thamani  Zaidi ya Shilingi Milioni Moja .
ACP Ngonyani Amesema Tukio Hili Limetokea Agosti 27 Mwaka Huu Majira ya Saa Nane Usiku na Hakuna Mtu Yoyote Aliyekamatwa Kuhusika na Tukio Hilo.
Hata Hivyo Jeshi La Polisi Mkoani Njombe Linaendelea na Upelelezi Juu ya Matukio Hayo Ambapo Amewataka Wananchi Kutoa Ushirikiano Kwa Kutoa Taarifa Kwenye Vyombo Vya Dola Ili Kuwabaini Watu Waliojihisisha na Vitendo Vya Uhalifu.
Blogzamikoa
 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa