Home » » Kevela Kamanda mpya UVCCM

Kevela Kamanda mpya UVCCM

Yono Stanley KevelaMBUNGE wa zamani wa Njombe, Yono Stanley Kevela  amechaguliwa kuwa Kamanda wa Umoja wa Vijana wa UVCCM wa Wilaya ya Wanging’ombe katika mkoa mpya wa Njombe.
Kevela ambaye aliwahi kuwa mbunge wa Njombe kati ya mwaka 2005-2010 anatarajiwa kusimikwa rasmi kwenye nafasi hiyo keshokutwa mkoani Njombe.
Akizungumza na gazeti hili mara baada ya uteuzi huo, Kevela aliwashukuru viongozi wote wa CCM kwa kumwamini na kusema kuwa amebaki na deni kubwa la kukitumikia chama hicho kwa uadilifu na uaminifu mkubwa.
“Nawashukuru wanaCCM wenzangu kuanzia ngazi ya mabalozi, tawi, kata, wilaya, mkoa hadi taifa kwa kuona ninafaa kukitumikia chama changu kwenye nafasi hii, nimebaki na deni la kukitumikia chama changu kwa unyenyekevu mkubwa na naahidi sitawaangusha,” alisema.
Kevela ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Yono Auction Mart, alisema wanachama wote wa CCM washikamane kutekeleza ilani ya chama chao na kuiga mfano wa Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Jakaya Kikwete namna anavyotekeleza ahadi kwa vitendo.
“Mheshimiwa Rais Kikwete ametekeleza ahadi zake kwa kiwango kikubwa sana, ameipaisha Tanzania chati katika anga za kimataifa, hivyo wanachama wengine lazima tufuate nyayo zake kwa kuchapa kazi na kukiimarisha chama, tusitegeane, kila mwanachama atimize wajibu wake,” alisema Kevela ambaye anasomea Shahada ya Uzamivu (PhD), katika Masoko, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Pia alisifu ziara zinazofanywa na Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana na timu yake katika mikoa mbalimbali kuwa ni hatua nzuri ya kukiimarisha na kukijenga chama hicho.
Kevela aliwashangaa baadhi ya viongozi wa chama hicho wanaojigeuza miungu watu kwa kushindwa kuwasikiliza wanachama wanapokuwa na kero mbalimbali.
“CCM ni ya wanachama, na viongozi hawapaswi kuwapuuzia wanapokuwa na jambo badala ya kujigeuza miungu watu na kuendesha mambo wanavyotaka wao,” alisema Kevela huku akisisitiza kwamba wapinzani wataambulia patupu uchaguzi wa 2015 kutokana na namna CCM inavyotekeleza ahadi zake kwa wananchi.
Alisema atatumia nafasi hiyo kuwasaidia vijana kupata fursa mbalimbali za kiuchumi kwenye taasisi za fedha ili waweze kupata fedha za kufanya ujasirimali na biashara hivyo kujiondoa kwenye lindi la umaskini.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa