Home » » Serikali yaombwa kuingilia ununuzi wa pareto

Serikali yaombwa kuingilia ununuzi wa pareto

WAKULIMA wa zao la pareto mkoani Njombe na Iringa, wameiomba serikali kuingilia kati ununuzi wa zao hilo kutokana na kuwapo kwa baadhi ya wanunuzi wanaowadhulumu wakulima kwa kuchezesha mizani na kuisafirisha nje.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wakulima hao wamesema hofu yao ni juu ya kuadimika kwa soko la pareto kama kiwanda kilichopo kitakosa malighafi kwa muda mrefu na kufungwa, hivyo kutaka wanunuzi wengi wawe wa ndani.
Walisema miaka ya nyuma kabla ya kuwapo kwa kiwanda hicho zao la pareto liliyumba kwa kukosa soko lakini tangu kiwepo Kiwanda cha PCT mjini Mafinga wamekuwa na uhakika wa kuuza zao hilo kwa wakati, tena bila kukopwa.
“Kuna wanunuzi wengi ambao wakiingia tu wanatangaza bei kubwa, lakini cha ajabu ukienda kupima kwao unashangaa fedha unayoipata ni ile ile ambayo inapatikana kwa kiwanda cha Mafinga, hii ina maana kuwa bei yao ipo juu kwa sababu wanajua kuwa wanachezesha mzani,” alisema Innocent Lukosi, mkazi wa Kijiji cha Iniho, wilayani Makete.
Aliiomba serikali kuhakikisha kuwa wanunuzi waliopo wanafuata sheria na taratibu badala ya kusafirisha zao hilo nje ya nchi wakati likiwa malighafi licha ya kuwepo kwa kiwanda.
Ofisa Tarafa wa Matamba, wilayani Makete, Benedict Mwageni, alisema wanahitaji ushindani kwenye soko la pareto lakini si kwa wanunuzi wasiofuata sheria na taratibu.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa