Home » » NANI WAMEIBA SH.480 BILIONI HAZINA

NANI WAMEIBA SH.480 BILIONI HAZINA

Tangu gazeti dada la The Citizen lichapishe mwishoni mwa wiki habari za upotevu wa Sh480 bilioni katika Wizara ya Fedha, Serikali imekaa kimya kama vile wizi huo ni tukio la kawaida, hivyo halihitaji maelezo ya kina wala ya haraka. Wananchi walitegemea kwamba Serikali ingetoa kauli haraka iwezekanavyo kuhusu mazingira ya upotevu huo na hatua inazochukua kuwawajibisha wahusika.
Tunasema kiasi hicho cha fedha zilizoibwa ni kikubwa kwa sababu ni zaidi ya bajeti ya mwaka kwa baadhi ya wizara, zikiwamo wizara kubwa kama ya Uchukuzi ambayo katika mwaka wa fedha wa 2013/14, kwa mfano ilitengewa Sh491 bilioni.
Tunaambiwa Sh480 bilioni zilizopotea katika Wizara ya Fedha zinaweza kujenga kilomita 375 za barabara kwa kiwango cha lami ikiwa ni urefu wa kutoka Dar es Salaam hadi Gairo, kilomita chache kutoka Dodoma. Tujiulize kiasi hicho cha fedha kingeweza kugharamia madawati, zahanati na madarasa mangapi kwa ajili ya wagonjwa na wanafunzi wetu.
Pamoja na ukimya wa Serikali kuhusu wizi huo, tumetiwa moyo na hatua ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Fedha za Serikali (PAC), ambayo imemtaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Fedha za Serikali (CAG), Ludovick Utouh kuchunguza upotevu huo wa kiasi hicho kikubwa cha fedha ambacho kilitumika pasipo maelezo katika kipindi cha miaka miwili ya fedha cha 2012/13 na 2013/14.
Wasiwasi wa kamati hiyo ni kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kuwapo kwa mtandao mkubwa wa wizi wa fedha za Serikali katika Wizara ya Fedha. Jambo hilo limethibitishwa na vitendo vya wizi wa kimtandao ambavyo vimekuwa vikifanywa na baadhi ya watumishi wake wakishirikiana na baadhi ya watendaji wa Tamisemi.
Ugumu uliopo hapa ni kwamba haijulikani kama fedha hizo zilizopotea zilitokana na kodi za wananchi au wafadhili ambao walichangia Sh842 bilioni katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2012/13. Ni sahihi kabisa kwa Kamati hiyo ya Bunge kushangazwa na kuendelea kuwapo kwa vitendo vya ufisadi serikalini, hasa kwa kuzingatia ukweli kwamba ripoti za CAG kila mwaka zimekuwa zikifichua wizi wa mabilioni ya fedha katika Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Kujirudia kwa vitendo hivyo kila mwaka ni ishara kwamba Serikali haina dhamira ya kupambana na vitendo hivyo.
Mwenendo huo wa Serikali unashangaza, hasa kutokana na ukweli kwamba mwaka 2013/14 ilikuwa na nakisi ya Sh847 bilioni katika bajeti yake. Hivyo, utekelezaji wa mipango yake ya maendeleo ingekwama kama siyo kukopa mabilioni ya fedha kutoka vyanzo vya nje na ndani ya nchi.
Matokeo yake ni kuzidi kuongeza mzigo wa Deni la Taifa ambalo limefikia Sh27 trilioni sasa, huku ikishindwa kukusanya kodi na kupanua wigo wa vyanzo vya kodi. Ndiyo maana iko hoi kifedha na karibu shughuli zake zote zimesimama, huku ikisuasua kulipa mishahara ya watumishi wake.
Pamoja na hali hiyo mbaya kifedha, bado vitendo vya wizi na ufisadi serikalini vinaendelea kama tunavyoshuhudia vikishamiri katika Wizara ya Fedha. Ni jukumu la Serikali kudhibiti ubadhirifu na ufisadi miongoni mwa watumishi wake, vinginevyo uchumi wetu utazidi kudidimia. Kwa kuanzia iwasake na kuwawajibisha wote walioiba Sh480 bilioni kutoka Hazina.
Chanzo;Mwananchi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa