Home » » MKUU WA WILAYA YA MAKETE AWAKUTANISHA POLISI NA MADEREVA WA BODABODA

MKUU WA WILAYA YA MAKETE AWAKUTANISHA POLISI NA MADEREVA WA BODABODA



 Kikao cha waendesha bodaboda kilichofanyika katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya Makete hii leo.
Mkuu wa wilaya ya Makete Mh. Josephine Matiro akionesha kitabu cha polisi kwa ajili ya kutoza faini za makosa ya usalama barabarani.
Mkuu wa polisi(OCD) wilaya ya Makete Alfred Kasonde akionesha risiti za faini ambazo zimetelekezwa na baadhi ya madereva ambao wengi wao wamekuwa wakilalamika kuwa fedha hizo zimeliwa na askari.
 Meneja Msaidizi wa TRA Makete Hamis Zumba akifafanua jambo kwa madereva bodaboda Makete.
 Dereva bodaboda aliyejitambulisha kama Alex akiuliza swali kwenye kikao hicho
 Mwalimu wa VETA Makete Bw. Mathew Komba akifafanua jambo kwenye kikao hicho

Na Edwin Moshi, Makete
Kutokana na ukosefu wa elimu ya sheria barabarani miongoni mwa madereva bodaboda wilayani Makete mkoani Njombe kunakopelekea madereva hao kukamatwa na askari wa usalama barabarani mara kwa mara, mkuu wa wilaya ya Makete Mh. Josephine Matiro amefanya kikao na waendesha bodaboda hao

Katika kikao hicho kilichofanyika kwenye ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya Makete, waendesha bodaboda hao walipata fursa ya kutoa kero zao na kuuliza maswali ambayo yalikuwa yakijibiwa papo kwa papo na Muu wa polisi wilaya ya Makete, askari wa usalama barabarani na Meneja msaidizi wa TRA Makete

Akizungumza kwenye kikao hicho Mkuu wa polisi wilaya ya Makete (OCD) Alfred Kasonde amekanusha vikali tuhuma zinazoelekezwa kwa askari wake kuwa wanakula fedha wanazotoza kama faini kwa vyombo vya usafiri wanavyotoza kutokana na makosa mbalimbali na kuongeza kuwa ni vingumu kwa askari ambaye amekuandikia faini ya kosa lako kwenye kitabu cha serikali kula fedha hiyo

Bw. Kasonde amesema askari wake hawana vitabu vya risiti na hawaruhusiwi kutembea navyo kwa kuwa jeshi la polisi lina wahasibu wanaokusanya fedha hizo, hivyo kwa wilaya ya Makete dereva akiandikiwa faini na askari, askari haruhusiwi kupokea fedha na badala yake atakuandikia karatasi maalum maarufu kama notification na baada ya hapo dereva huyo atakwenda kulipa faini hiyo kituoni

Amewataka madereva hao kuacha kuwapa fedha ya faini askari hao na badala yake wahakikishe askari aliyewakamata anaandika kosa hilo kwenye kitabu cha faini, huku akionesha rundo la risiti za madereva bodaboda ambao wamelipia faini lakini hawajafika kuchukua risiti zao kwa madai kuwa fedha walizotoa zililiwa na askari

Kwa upande wake mkuu wa wilaya ya Makete mh. Josephine Matiro amewataka madereva hao kuhakikisha wanajikamilisha kwa vitu vyote vinavyohitajika kama sheria za usalama barabarani zinavyolelekeza ili kuepukana na adha ya kukamatwa mara kwa mara na askari na kutozwa faini

Mh Mariro amesema ni kweli madereva wengi hawajui sheria za usalama barabarani lakini sheria hazitambui kuwa hawafahamu sheria, hivyo ili kuepukana na adha hiyo wanatakiwa kuwa na vitu vyote vinavyohitajika kama leseni ya udereva, leseni ya biashara, bima, kadi ya pikipiki, stika ya nenda kwa usalama, kofia ngumu(helment 2) pamoja na pikipiki yenye vyake vifaa vyote

Amesema kwa kulitambua hilo mkuu huyo atafanya mazungumzo na chuo cha VETA Makete kifanye mafunzo maalum kwa madereva hao kwa gharama nafuu ili wazifahamu sheria za usalama barabarani pamoja na kupata leseni za udereva

Katika kikao hicho madereva hao walikuwa wakiuliza maswali mengi ya ufahamu ambapo walijibiwa maswali yao yote na kuondoka kwa furaha na uelewa wa mambo mbalimbali ya usalama barabarani

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa