Home » » CHADEMA yawatoa hofu wafanyakazi

CHADEMA yawatoa hofu wafanyakazi

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimewataka wafanyakazi wa serikali na umma nchini kote kuondoa hofu ya kukosa ajira endapo chama hicho kitaingia madarakani baada ya Uchaguzi Mkuu mwakani.
Hayo yamebainishwa jana na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willibrod Slaa, katika hotuba zake kwenye mikutano tofauti ya Operesheni M4C Pamoja Daima inayoendelea nchini kote, yenye lengo la kuwaunganisha Watanzania kuelekea chaguzi zijazo, ukiwemo Uchaguzi Mkuu.
Akifafanua zaidi kuhusu hofu iliyojengeka kwa wafanyakazi wengi nchini kutokana na propaganda zinazoenezwa na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), alisema kuwa kamwe chama hicho hakitawabagua au kuwaondoa kazini wafanyakazi wa serikali, kwa sababu tu walikuwa kwenye serikali iliyokuwepo madarakani.
“Ni mtu mwenye akili finyu tu ndiye anaweza kufikiria hivyo, kwa sababu CHADEMA kaiwezi kuongoza kuwaondoa wafanyakazi wa serikali waliopo sasa na kutegemea wafanyakazi wapya, wapo wanaosema eti  CHADEMA ikiingia madarakani watatoa wapi wafanyazi, au Ikulu wataipata wapi, hao waliopo ambao ni wasafi ndio watakaoendeleza gurudumu,” alifafanua.
Alisema Ikulu iliyopo si mali ya CCM au chama chochote ni mali ya serikali na kiongozi atakayechaguliwa kutoka chama chochote atakwenda Ikulu hiyo hiyo na wafanyakazi waliopo ndio watakaoendelea kuitumikia serikali hiyo mpya.
“Kwa hiyo nawataka wafanyakazi wote nchini wakiwemo askari polisi na wanajeshi waondoe hofu hiyo, tutakachofanya ni kuchuja wafanyakazi waadilifu na wasio waadilifu, kwa mfano askari polisi ambaye ni mla rushwa au mfanyakazi ambaye ni fisadi, hatutakuwa naye,” aliongeza.
Katika hatua nyingine, Dk. Slaa amemtaka Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, kutekeleza kauli yake aliyoitoa hivi karibuni kwamba serikali itamega sehemu ya ardhi aliyopewa mwekezaji katika mashamba ya mpunga mkoani Mbeya ili kuwarudishia wananchi ambao wanahangaika kutafuta ardhi ya kilimo.
Alisema serikali mara nyingi imekuwa na kauli zisizotekelezeka, hivyo kuwafanya wananchi kutokuwa na imani na serikali yao.
Aidha, katika hotuba zake hizo, Dk. Slaa amemtaka Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi, kukemea na kuchukua hatua kwa vyama ambavyo vinaweka makambi ya kuwafundisha vijana wao kufanya vurugu, ikiwamo kupiga watu wakati wa uchaguzi.
Alisema CHADEMA kimekuwa chama kivumilivu sana kutokana na vurugu hizo ambazo mpaka sasa zinafanyika katika baadhi ya miji, jambo ambalo linahatarisha amani nchini.
“CHADEMA hatuamini katika vurugu, lakini tuna uwezo wa kujitetea, vijana wetu wamepigwa na wengine kupoteza maisha kutokana na vurugu zinazofanywa na vijana wanaoitwa Green Guards, tunaamini msajili aliyepo sasa atalifanyika kazi jambo hili, kama mnavyojua  hata hapa Mbeya yapo makambi ambayo yanaendelea kutoa mafunzo hayo,” aliongeza
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa