Home » » USHIRIKIANO KATI YA EPZA,KOREA KUIMARISHWA ZAIDI

USHIRIKIANO KATI YA EPZA,KOREA KUIMARISHWA ZAIDI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

SERIKALI ya Tanzania kupitia Mamlaka ya U kanda Maalumu wa Uwekezaji nchini (EPZA), inatarajia kuanza kupata wawekezaji wengi kutoka Jamhuri ya Korea Kusini kwa faida ya nchi zote mbili.
Matarajio hayo yanatokana na ziara iliyofanywa hivi karibuni na wawekezaji katika mamlaka hiyo na kujionea maeneo maalumu ya uwekezaji na fursa zinazopatikana katika maeneo hayo.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Dkt. Adelhelm Meru, hatua hiyo ni muhimu kwa nchi hizo mbili katika kuimarisha uchumi na uwekezaji endelevu.
Ujumbe huo ulijumuisha wafanyabiashara wakubwa kutoka kampuni 22 za nchi hiyo.
"Wamekuja na ujumbe mkubwa sana na tunatarajia sasa kuanza kupata wawekezaji wengi kutoka nchi hii," alisema Dkt. Meru.
Ujumbe wa wafanyabiashara hao uliongozwa na balozi wa nchi yao nchini Tanzania, Chung H na ilikuwa ni mara ya kwanza kwa kundi kubwa la wafanyabiashara wa nchi hiyo kuja nchini.
"Sisi tulitumia nafasi hii kuwaonesha vivutio ambavyo vinarahisisha biashara na uwekezaji katika maeneo yetu," alisema. Pia walioneshwa fursa zilizopo katika maeneo ya mamlaka zikiwemo za kuanzisha viwanda vya kuongeza thamani mazao ya kilimo na madini kwa ajili ya masoko ya nje.
Fursa nyingine zilizotajwa zilikuwa za ujenzi wa miundombinu ya nishati, maji na utoaji wa huduma mbalimbali katika maeneo maalumu ya mamlaka hiyo yaliyopo katika mikoa 20 hapa nchini.
Alisema maeneo maalumu ya vipaumbele ni pamoja na Bagamoyo, Mtwara na Kigoma ambayo yana fursa nyingi.
 "Kwa bahati nzuri tumekuwa tukifanya nao kazi kwa muda mrefu na tunajua wao ni mabingwa wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA)," alisema.
Naye Balozi Chung H, alisema nchi yake inauhusiano mzuri na Tanzania na ziara ya wafanyabiashara wa nchi yake inadhihirisha uhusiano huo.
"Tunahitaji kuzidi kuongeza ushiriki wa wafanyabiashara wetu kufanya biashara na nchi hii ya Tanzania," alisema.
Mkuu wa ujumbe wa wafanyabiashara hao, Lee Kang Min, alisema wamekuja nchini Tanzania kwa ziara ya kuangalia mazingira ya uwekezaji na wamefurahi kuona fursa nyingi zilizopo.
"Tutarudi kuwekeza," alisema na kuongeza kuwa wafanyabiashara hao waliridhika na hali halisi ya mazingira ya uwekezaji na fursa zilizopo Tanzania. Wafanyabiashara hao pia walifanya ziara katika kiwanda cha nguo kilicho katika eneo la mamlaka hiyo cha Tanzania Tooku Garments Co. Ltd.

Chanzo:Majira

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa