Home » » WAAJIRI WATAKIWA KULINDA AFYA ZA WAFANYAKAZI

WAAJIRI WATAKIWA KULINDA AFYA ZA WAFANYAKAZI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

SERIKALI imewataka waajiri wote kuhakikisha wanaanzisha mifumo bora mahali pa kazi itakayohakikisha wafanyakazi wao wana usalama na wenye afya bora.
Alisema suala hilo si jambo la hiari kwani linagusa uhai na maisha ya watu.Akizungumza kwenye maadhimisho ya siku ya afya na usalama mahali pa kazi Duniani, Makamu wa Rais, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, aliwataka waajiri wasikwepe wala kuogopa gharama katika hilo.
"Zingatieni kuwa hakuna kitu chenye thamani kuzidi uhai na maisha ya watu," alisema.
Alisema takwimu za Shirika la Afya Duniani (ILO) zinaonesha kuwa Kila mwaka duniani takriban watu milioni 337 hupata ajali kazini na kati yao wafanyakazi milioni 2.3 hufariki kutokana na ajali na magonjwa yatokanayo na kazi wanazofanya.
"Takwimu zinatuonesha kuwa watu wanaofariki kutokana na magonjwa ya ajali kazini ni wengi kuliko wale wanaofariki vitani, ni wazi kuwa ajali nyingi na magonjwa kazini hutokana na wafanyakazi kutozingatia kanuni za usalama na afya kazini na waajiri kutochukua hatua za kupunguza ajali na magonjwa hayo," alisema Dkt. Bilal.
Alisema kila mfanyakazi anastahili kufanya kazi yenye ujira wa kutosha kukidhi mahitaji ya msingi katika mazingira salama bila kuhatarisha afya yake, kinyume na hapo kazi hiyo haitakuwa ya staha na haipaswi kufanywa na binadamu yeyote, inayostahili kupigwa marufuku.
Hata hivyo, alisema siku ya usalama na afya mahali pa kazi duniani ni siku muhimu kimataifa ambapo nchi zote wanachama wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) tangu mwaka 2001 zilitakiwa kuadhimisha siku hiyo.
Pia alisema maadhimisho hayo yanatoa fursa ya kubainisha njia mbalimbali za kuzuia magonjwa na ajali zinazotokea kazini na kuimarisha kampeni za kuboresha usalama afya na ustawi wa wafanyakazi wakiwa kazini.
Alisema Serikali inafanya juhudi kubwa kuhakikisha inadhibiti matumizi yasiyofaa ya kemikali sehemu za kazi na maeneo mengine kwa manufaa ya afya na wananchi wake.
"Pamoja na juhudi zinazofanywa na Serikali madhara ya kemikali yameendelea kuathiri jamii yetu kwa njia moja au nyingine na haya yanachangiwa na tabia za baadhi ya watu wasio waungwana miongoni mwa jamii," alisema Dkt. Bilal. Alisema Serikali itaendelea kusimamia na kudhibiti matumizi mabaya ya kemikali kwa kutoa elimu kwa watumiaji na wananchi kuhusu matumizi sahihi na madhara yatokanayo na matumizi mabaya ya kemikali.

Chanzo;Majira

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa