Home » » MAONI:RIPOTI YA CAG HAITOI MATUMAINI YOYOTE

MAONI:RIPOTI YA CAG HAITOI MATUMAINI YOYOTE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka wa fedha wa 2012/13 imefichua madudu ya ajabu, ambayo bila shaka yatakuwa yameondoa matumaini ya wananchi ya kukua kwa uchumi na kuwaondolea umaskini uliokithiri. Ripoti za CAG za miaka ya fedha iliyopita zilikuwa pia zinafichua madudu ya kutisha, lakini baada ya Serikali kuahidi kwamba ingeepuka kurudia madudu hayo na kuzifanyia kazi changamoto nyingi zilizokuwa zikiibuliwa na ripoti mbalimbali za CAG, wananchi wengi walipata matumaini.
Inasikitisha kwamba ripoti hiyo iliyotolewa ufafanuzi na CAG mwenyewe, Ludovick Utouh juzi, imeonyesha dhahiri  kwamba Serikali haijawa na dhamira ya kweli ya kudhibiti matumizi mabaya ya fedha za Serikali na kupambana na vitendo vya ufisadi na ubadhirifu wa mali ya umma. Pamoja na kuwapo kwa Bunge na mifumo mingine kadhaa ya kuhakikisha kwamba Serikali inakuwa na nidhamu katika kusimamia mapato na kudhibiti matumizi yake, bado hakuna mabadiliko wala dalili za uwajibikaji katika matumizi ya fedha za Serikali.
Ripoti ya CAG inaonyesha kwamba matumizi hayo mabaya yanaendelea pamoja na hali mbaya ya uchumi inayolikabili taifa. Kwa mwenendo huo, inaonekana hakuna uwezekano wa kupunguza Deni la Taifa ambalo lilifikia Sh21.20 trilioni, ambalo ni ongezeko la Sh4.23 trilioni sawa na asilimia 25, ikilinganishwa na Sh16.98 trilioni katika mwaka wa fedha wa 2011/12. Ndani ya Serikali umekuwamo utamaduni wa ufujaji wa fedha tunaoweza kusema ni wa mashindano, ambao umechangia kupanda kwa deni la ndani kutoka Sh4.55 trilioni mwaka 2011/2012 hadi Sh5.78 mwaka wa 2012/13, likiwa ni ongezeko la Sh1.23 trilioni, sawa na asilimia 27.
Mwenendo huo ni hatari kwa uchumi na maendeleo ya taifa letu. Baya zaidi ni pale Serikali inapoendekeza mikopo kutoka katika benki za biashara nje ya nchi. Ripoti ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), inasema kwamba Serikali imekuwa ikikopa wastani wa Sh360 bilioni kwa mwezi kutoka nje. Kutokana na hali hiyo,  Shirika la Fedha Duniani (IMF) na Benki  ya Dunia (WB), vimeonya dhidi ya mwenendo huo kwamba utahatarisha uchumi, ingawa Ripoti ya CAG inasema mikopo hiyo imesaidia miradi mikubwa ya maendeleo kama uboreshaji wa miundombinu na kadhalika.
Sisi hatudhani kama mikopo hiyo ina madhara kwa uchumi iwapo utakuwapo uwazi na itasimamiwa kwa uadilifu, kwa maana ya kuhakikisha kwamba siyo tu unakuwapo usimamizi katika  matumizi ya fedha hizo, bali pia zinatumika kuendesha miradi iliyokusudiwa. Miradi mingi ya maendeleo imekuwa ikikwama kutokana na fedha zake kuingizwa katika michepuko isiyofaa, mbali na wizi na ubadhirifu wa baadhi ya wanasiasa, watendaji wa Serikali na taasisi zake.
Ripoti ya CAG imebaini ufisadi mkubwa katika maeneo mengi ya mapato na matumizi ya fedha za Serikali. Kwa mfano, magari mapya 11 yenye thamani ya mamilioni ya shilingi yalinunuliwa lakini yaliishia katika miliki za watu binafsi. Sh1.62 zililipwa kama mishahara kwa watumishi hewa, huku misamaha ya kodi ikilipotezea taifa Sh1.52 trilioni ambazo zingeweza kujenga shule za sekondari za kisasa zaidi ya 300. Ripoti ya CAG haitoi matumaini. Serikali isipopambana na ufisadi na ubadhirifu wa mali ya umma, maendeleo na ustawi wa jamii nchini utabaki kuwa ndoto za mchana.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa