Home » » WAKULIMA WAHAMASISHWA KUUNDA VIKUNDI

WAKULIMA WAHAMASISHWA KUUNDA VIKUNDI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

KITUO maalumu cha uendelezaji kilimo Ukanda wa Kusini mwa Tanzania (SAGCOT) kimetoa wito kwa wakulima wadogo kuungana kwa kuunda vikundi vidogo ili kuirahisishia Serikali kuwafikishia huduma muhimu za pembejeo na mikopo katika kuinua sekta hiyo hapa nchini.

Wito huo ulitolewa jana na Ofisa Mtendaji Mkuu wa kituo hicho, Geoffrey Kirenga, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mada alizotarajia kuziwasilisha kwenye mkutano wa wadau wa Umoja wa Watendaji Wakuu wa Kampuni (CEOrt).

"Mkiungana pamoja inakuwa rahisi kuwapatia mafunzo na kuwawezesha kupata mikopo, kwa sababu jukumu letu ni kuwatafutia masoko na kuwawezesha wakulima hawa kuongeza uzalishaji," alisema kirenga.

Aidha alitoa wito kwa wawekezaji na kampuni binafsi kuwekeza kwenye sekta ya kilimo katika ukanda huo kwa kuwa ni ukanda ambao una hali ya hewa nzuri inayostawisha vyema mazao mbalimbali yanayotakikana.

"Kwa mfano maeneo ya Mkoa wa Iringa wanalima pia viazi, awali walikuwa wakivuna kuanzia tani 5 hadi 7 kwa mwaka lakini baada ya kutafuta wawekezaji na kuwasaidia wakulima wadogo na wa kati, sasa wanavuna tani 25 hadi 30 za viazi.

Alisema ukanda huu unazalisha mazao ya chakula na biashara kwa asilimia 65 nchini, sasa iwapo zikitumiwa ipasavyo fursa zilizopo katika ukanda huu hawawezi kuhangaika hata kidogo.

"Kwa sababu tulijaribu katika shamba la mpunga hapo Kilombero kwa kutafuta mwekezaji ambaye aliwasaidia wakulima, na sasa matunda yanaonekana kwani wanavuna tani 5.6 za mpunga kutoka tani moja za awali walizokuwa wakivuna," alisema Kirenga.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CEOrt, Ali Mufuruki alisema jukwaa hilo litaendelea kuwakutanisha wataalamu mbalimbali na maofisa watendaji wakuu wa makampuni ambao ni wanachama ili kuisaidia serikali kujikwamua kiuchumi.

Alisema ndani ya jukwaa hilo la CEOrt kuna kampuni zaidi ya 100 ambazo kwa hakika zikitumiwa vyema zinaweza kuinufaisha jamii inayowazunguka

Chanzo;Majira

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa