Home » » Sera ya Ajira kupitiwa upya

Sera ya Ajira kupitiwa upya



SERIKALI inapitia upya Sera ya Taifa ya Ajira ya mwaka 2008 ili kuangalia changamoto zilizomo. Mapitio hayo yatakamilika kabla ya Desemba, mwaka huu, lengo likiwa kutoa fursa kwa wadau kushirikiana na serikali katika suala zima la ajira nchini.
Mkurugenzi wa Ajira kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana na Ajira, Ally Msaki alisema hayo jijini Dar es Salaam hivi karibuni na kuongeza kuwa hatua ya kuipitia sera hiyo, inatokana na kuwapo kwa mabadiliko mbalimbali.
Alisema, serikali itafanya kila linalowezekana, kuhakikisha kunakuwepo sera, sheria pamoja na kanuni rafiki, kwa maendeleo ya programu zinazokuza ujuzi na ajira kwa vijana.
“Sera hiyo imekuwa ikipitiwa na Taasisi ya Utafiti ya Kuondoa Umaskini (Repoa) na tayari ripoti inayoelezea hali halisi, imeshajadiliwa na wadau na sasa hivi wanaandika sera yenyewe,” alisema Msaki.
Alisema wadau, wameshiriki katika kuipitia sera hiyo, kazi kubwa imefanyika na imeangalia changamoto na matatizo mbalimbali yanayoikabili sera hiyo ili itakapokamilika itatoa mwanga wa wadau wengine kushirikiana na serikali katika suala la ajira.
Msaki alisema serikali itaendelea kusimamia sera hiyo ya elimu na mafunzo ya ufundi stadi, kwa lengo la kuweka msisitizo katika kuandaa mazingira na kutoa elimu ya ufundi stadi katika ngazi mbalimbali kuendana na mahitaji ya soko la ajira na hatimaye kuongeza ajira nchini.
Kuhusu mipango ya serikali katika juhudi za kukuza ajira, ni pamoja na kuimarisha utekelezaji wa mfuko wa maendeleo ya vijana ambao unalenga kuwasaidia vijana kujiajiri na kuwapa mikopo ya masharti nafuu na mafunzo ya ujasiriamali.
Alisema serikali itajikita katika kuhamasisha na kuwezesha uwekezaji kwenye viwanda vidogo, vya kati na vikubwa ili kufikia lengo la asilimia 40 ya nguvukazi nchini kuwa katika sekta ya viwanda ifikapo mwaka 2020, kulingana na mpango wa pili wa maendeleo wa miaka mitano kuanzia 2016/17 hadi 2020/21.

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa