Home » » USAFI POLISI WAPONZA CHADEMA

USAFI POLISI WAPONZA CHADEMA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Makamu Mwenyekiti wa Chadema Nyanda za Juu Kusini, Alatanga Nyagawa

Jeshi la Polisi mkoa wa Njombe juzi liliwashikilia kwa saa tatu wafuasi na viongozi  wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wilaya ya Njombe kwa tuhuma za kuingia kwa jinai kwenye kambi yake.

 Makamu Mwenyekiti wa Chadema Nyanda za Juu Kusini, Alatanga Nyagawa, alidai kuwa viongozi na wafuasi hao walitiwa mbaroni  baada ya kuingia kwenye kambi hiyo kwa lengo la kufanya usafi kwenye makazi ya askari na kituo cha polisi ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya siku ya kumbukumbu ya Nyerere maarufu kama Nyerere Day.

Alisema wafuasi hao na  Diwani wa Kata ya Njombe Mjini, Agrey Mtambo, mwenyekiti wa wilaya, kamanda wa vijana mkoa, na katibu wake walikamatwa na kupelekwa kituoni na kwamba waliachiwa baada ya kuhojiwa.

Aliyataja maeneo mengine ambayo walipanga kufanya usafi kuwa ni masoko ya mjini, kituo cha mabasi.

Alisema  ratiba yao ilionyesha kwamba walitakiwa kuanza kufanya usafi katika kambi hiyo ya polisi, kituo cha polisi na mkoa, mahakama na hospitali teule ya wilaya ya Njombe ya Kibena.

Hata hivyo hawakuweza kukamilisha zoezi hilo kutokana na kutiwa mbaroni. 

Kamanda  wa Polisi mkoa wa Njombe,  Fulgence Ngonyani, alithibitisha kukamatwa kwa viongozi hao hao baada ya kuingia kwenye kambi ya jeshi hilo bila ya kuwa na kibali wala kutoa taarifa

Kamanda Ngonyani alisema watuhumiwa hao wana kosa la jinai kwa kuvamia eneo la jeshi hilo bila kutoa taarifa na kuwa watafikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa