Home » » Sara Dumba kuzikwa kesho

Sara Dumba kuzikwa kesho

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Sara Dumba enzi za uhai wake
MKUU wa Wilaya ya Njombe, Sara Dumba aliyefariki ghafla juzi jioni, anatarajiwa kufanyiwa ibada leo mjini Njombe na kuagwa rasmi na wananchi wa wilaya hiyo na Mkoa wa Njombe na baadaye jioni kusafirishwa kuja jijini Dar es Salaam ambako ndiko atakapozikwa.
Kwa mujibu wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Njombe, Jackson Saikadau, ratiba ya awali inaonesha kuwa Dumba anatarajiwa kuzikwa kesho nyumbani kwake eneo la Mbutu Mwembe Mdogo Kigamboni na msiba wake utafanyika Kigamboni nyumbani kwa baba yake mzazi eneo la Ferry Midizini.
Saikadau alisema ratiba hiyo inaonesha kuwa mwili wa marehemu ambao baada ya mauti ulihifadhiwa katika Hospitali ya Ilembula, utawasili mjini Njombe saa nne asubuhi kwa ajili ya ibada na baadaye kuagwa na wananchi.
“Tunatarajia kuanza safari majira saa 10 jioni kutoka Njombe kwenda Dar es Salaam na maiti itawasili jijini humo alfajiri siku ya Alhamisi (kesho) kwa ajili ya taratibu za msiba na mazishi,” alisema Saikadau. Alisema Dumba alifariki ghafla juzi baada ya kusumbuliwa na tatizo la shinikizo la damu.
Alisema kabla ya mauti, alilalamika kusumbuliwa na kichwa na hivyo kukimbizwa katika Hospitali ya Kibena, lakini pamoja na jitihada za madaktari za kuokoa maisha yake, alifariki dunia majira ya saa moja na nusu usiku.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Makete, Daudi Yassin alisema mkoa umepata pigo kwa kuondokewa na Dumba ambaye katika uhai wake ndiye aliyekuwa Mwenyekiti wa Wakuu wa Wilaya wa mkoa huo wa Njombe.
“Kwa kweli huu msiba umetushtua sana, kwani Jumamosi iliyopita tulikuwa na Dumba katika sherehe za kumpokea Mkuu wetu wa Mkoa, Rehema Nchimbi baada ya kuapishwa, kwa kweli mchango wake utakumbukwa sana,” alisema Yassin.
Kitaaluma Dumba ni Mwandishi wa Habari aliyekuwa mtangazaji wa iliyokuwa Radio Tanzania ambao kwa sasa inajulikana kama Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).
Aidha, alishika nyadhifa mbalimbali za ukuu wa wilaya katika maeneo tofauti zikiwemo wilaya za Kilindi na Njombe alikofikwa na mauti.
Katika hatua nyingine, Rais John Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Njombe, Dk Rehema Nchimbi kutokana na kifo cha ghafla cha Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sara Dumba.

Chanzo Gazeti la Habari leo

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa