Home » » NGOMBE WA MILIONI 400/- WAPOTEA NARCO

NGOMBE WA MILIONI 400/- WAPOTEA NARCO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mwenyekiti wa PAC,Deo Filikunjombe.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), imesema Shirika la Ranchi za Taifa (Narco), halistahili kupewa Sh. bilioni 17 walizoomba serikalini kutokana na kushindwa kusimamia uendeshaji na upotevu wa ng’ombe 376 katika Ranchi ya Ruvu mkoani Pwani.

Mwenyekiti wa PAC, Deo Filikunjombe, jana alitoa maelekezo ya kamati kwa viongozi wa Narco na Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, baada ya kuwahoji juu ya taarifa ya ukaguzi maalum iliyofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Alisema ukaguzi huo ulibaini kuwa ngombe 376 wamepotea kwa kipindi cha miezi mitatu, makato ya mifuko ya hifadhi ya jamii ya wanachama haipelekwi, kushindwa kuendelea kwa ujenzi wa machinjio licha ya serikali kutoa fedha na kuendelea kudidimia kwa Shirika hilo siku hadi siku.

Ng’ombe hao wana thamani ya Sh. 413,600,000 ikiwa kama kila ng’ombe atakuwa na kilo 220 na kuuzwa kwa Sh. 5,000 kwa kilo moja.

“Kamati tumeona hamstahili kupewa fedha hizi kutokana na kushindwa kwa menejimenti, fedha nyingi imepotea na mifugo pia imepotea, hatupendekezi mpewe fedha hadi mbadilike,” aliagiza Filikunjombe.

Mwenyekiti wa Bodi ya NARCO, Salum Shamte, aliieleza kuwa shirika linakabiliwa na tatizo la ukosefu wa mtaji wa kujiendesha, miundombinu duni jambo ambalo ni gumu kutengeneza faida.

Alisema Narco ilichukua mkopo katika benki ya  CRDB ambako riba ni kati ya asilimia 16 na 18 na kwmba kwa mkopo wa Sh. milioni 400 walilipa Sh. milioni 700 na kwmaba mkopo wa benki ya TIB ni wa kununua ng’ombe na kunenepesha ambao hauwezi kulivusha shirika hilo.

Shamte alisema ujenzi wa machinjio ulisitisha baada ya kuingia mkataba na Suma JKT ambao walijenga chini ya kiwango na kuvunja mkataba nao na kwamba ujenzi utaendelea siku za karibuni na unatarajiwa kukamilika mwakani.

Baada ya maelezo hayo, kamati hiyo iliagiza Msajili wa Hazina kupitia taarifa ya uchunguzi ya CAG akishirikiana na Wizara na kuchukua hatua kwa kipindi cha wiki tatu.

Pia, Bodi ya NARCO ijitathmini iwapo menejimenti ya Narco Taifa na Ruvu, zinastahili kuendelea kuwepo na umri wa kustaafu ni miaka 60, lakini Mkurugenzi Mkuu ana miaka 61. Mwenyekiti wa Bodi pia ametakiwa kujitathimini kama anastahili kuendelea kuwepo.
SOURCE: NIPASHE

0 comments:

Post a Comment

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Njombe Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa